Kessy vs Juma Abdul Mbona patachimbika
NA ZAITUNI KIBWANA
HAPANA shaka kwa sasa Juma Abdul, Hassan Ramadhan ‘Kessy’ na Shomari
Kapombe ndio mabeki wa kulia bora nchini, wamethibitisha ubora wao Ligi
Kuu Bara na hata katika michezo ya kimataifa ya timu zao na Taifa Stars
kila walipopata nafasi ya kucheza.
Nani asiyejua uwezo wa Abdul, Kessy na Kapombe? Kwanini tusifananishe
uwezo wao na nahodha wa zamani wa timu ya Taifa ya Brazil, Marcois
Evangelista de Morais ‘Cafu’ au Danny Alves?
Uwezo wao wa kupandisha mashambulizi kwa timu pinzani, kucheza kwa
kasi ya hali ya juu mwanzo mwisho kumewafanya kuonekana kama ni beki
mwenye mapafu ya mbwa.
Kimsingi naweza kusema kwa hivi sasa Tanzania kuna mabeki watatu wa
kulia ambao wamemfanya kocha wa timu ya Taifa ya Tanzania, Charles
Boniface Mkwasa, kukenua meno kila mara aitapo wachezaji wa kuunda
kikosi cha timu ya Taifa.
Uwezo wao wa kupandisha mashambulizi, kupiga krosi, kurusha mipira
hizi ni sifa zinazoendelea kuwakosha mashabiki mbalimbali wa timu zao.
Baada ya kila mmoja kuwa kwenye himaya yake, Juma Abdul (Yanga),
Kapombe (Azam) na Kessy (Simba) na kugombea namba wanapokutaka kwenye
timu ya taifa tu, sasa mambo yamebadilika na Abdul na Kessy wamejikuta
wakiingia kwenye vita mpya ya namba Jangwani.
Hii ni baada ya Kessy kusajiliwa Yanga akitokea Simba na moja kwa
moja kuhamishia ile vita ya nani acheze kwenye kikosi cha kwanza cha
Stars pale anapokosekana Kapombe katika makutano ya mtaa wa Jangwani na
Twiga.
Kessy aliyesajiliwa na Simba akitokea kwa wakata miwa wa Turiani,
Mtibwa Sugar amejizolea umaarufu mkubwa kwa muda mchache alioichezea
Simba na hii inatokana na kiwango bora alichokionyesha licha ya umbo
lake la kawaida.
Ni mchezaji mwenye pumzi ya kutosha na ni mzuri wa kukaba na
kuipandisha timu mbele na ni mpishi mzuri wa magoli, sababu ambayo
imepelekea mashabiki kumfananisha na nyota wa Barcelona, Dani Alves.
Tofauti na wachezaji wengi wa hapa Tanzania, Kessy anajiamini sana
akiwa uwanjani na hata nje ya uwanja hakika kijana huyu ameitendea haki
jezi yake namba 4 ambayo ameichagua kuivaa jezi ambayo imewahi kuvaliwa
na wakali wengi waliopitia katika klabu ya Simba akiwemo mlinzi Victor
Costa Nampoka.
Kutokana na uwezo wao kufanana wakiwa na timu zao, BINGWA leo linachambua uwezo wa wachezaji hao huku kwa upande wa Kessy na Abdul ambao sasa watakuwa kwenye timu moja.
Kutokana na uwezo wao kufanana wakiwa na timu zao, BINGWA leo linachambua uwezo wa wachezaji hao huku kwa upande wa Kessy na Abdul ambao sasa watakuwa kwenye timu moja.
Ni vyema tukaangalia vigezo muhimu vinavyoweza kutuongoza
kuwalinganisha ili kufahamu ubora wao, labda mifumo ya timu zao nayo
inafaa kuangaliwa kwani mara nyingi ndiyo inayomwelekeza beki nini
afanye na kwa wakati gani.
Unapoiangalia Yanga inayopenda mfumo wa 4-4-2 unagundua kuwa mfumo
huu unategemea sana viungo wa kati na pembeni kuwachezesha washambuliaji
wa kati kujipatia magoli hapa ndipo unapopata picha kuwa mashambulizi
ya Yanga hutengenezwa kutoka kwa Thabani Kamusoko, Simon Msuva, Geofrey
Mwashiuya, Deus Kaseke na Malimi Busungu na hivyo Yanga hawategemei sana
krosi za mabeki wa pembeni labda itokee tu.
Kwa hali hiyo, Juma Abdul hana fursa nyingi zinazomsogeza karibu na
goli ili azitumie na kufunga isipokuwa kwa kutumia uwezo wake wa kupiga
mashuti ya mbali kufunga magoli, ingawa nafasi hizo hazitokei mara kwa
mara na kumwacha ategemee mipira ya adhabu kubwa.
Katika ulinzi itakuwa rahisi kwake kuihami timu vizuri, muda mwingi haondoki katika nafasi yake isipokuwa kwa nadra.
Asilimia kubwa ya magoli ya Yanga yanatengenezwa upande huo na pia ana uwezo mkubwa wa kupiga mashuti na krosi. Ukiachana na michezo ya ligi kuu, Abdul ameonyesha kiwango maridhawa katika mechi ngumu za kimataifa mwaka huu!
Asilimia kubwa ya magoli ya Yanga yanatengenezwa upande huo na pia ana uwezo mkubwa wa kupiga mashuti na krosi. Ukiachana na michezo ya ligi kuu, Abdul ameonyesha kiwango maridhawa katika mechi ngumu za kimataifa mwaka huu!
Hakika vijana hawa wamejitahidi sana na kuonyesha kuwa wanaweza kuja
si kuziba tu ile nafasi ya Nsajigwa katika timu ya taifa, bali
kuifikisha mbali zaidi timu yetu ya Taifa ya Tanzania na hususani klabu
zao.
Kwa Kapombe sote tunaweza kukumbuka aina yake ya uchezaji kama mlinzi
alipokuwa Simba, alitumia muda mwingi kukaba na muda mchache
kushambulia hata mabao yake ya kufunga yalikuwa machache.
Wakati Kapombe inapobidi kukaba anafanya hivyo kwa bidii na uwezo
mkubwa. Kwa sasa si rahisi kwake kuonekana hivyo kama zamani kutokana na
mfumo wa Azam wa 3-5-2 huku yeye akipewa uhuru (Free role) kunyatia
matundu yanayojitokeza ndani ya eneo la hatari la timu pinzani, kuiwahi
mipira inayozagaa na hivyo kufunga magoli muhimu kwa timu yake ambayo
huenda yakamfanya aweke rekodi ya beki aliyefunga mabao mengi katika
ligi yetu na ligi zote za ukanda huu wa Afrika, manane (8) hadi sasa.
Lakini wakati Kapombe akitakata kwenye mfumo wa 3-5-2, ni wazi kuwa
Kessy na Abdul wataendelea kutumika kwenye mfumo wa 4-4-2 ambao hupendwa
zaidi na kocha Hans van der Pluijm.
Kessy na Abdul wote wana sifa ya kupandisha timu na kushiriki kwenye
kutengeneza nafasi na ndiyo maana Abdul amehusika kwenye sehemu kubwa ya
mabao ya Yanga na ndivyo hivyo hivyo Kessy amefanya kwenye kikosi cha
Simba.
Tafauti pekee kati yao hasa kwenye idara ya kushambulia ni ukweli
kuwa Abdul huwa ana maamuzi mazuri zaidi ya mwisho kuliko Kessy ambaye
wakati mwingine huonekana kukosa umakini na kushindwa kumalizia vizuri
kazi kubwa ambayo anaweza kuwa ameifanya.
Na ndiyo maana Juma Abdul amekuwa mfungaji mzuri zaidi ya Kessy
kwenye msimu huu hii ni kutokana na utulivu wake anapokuwa mbele na
mpira.
Lakini ukirudi kwenye idara ya ukabaji ni wazi kuwa wote ni mabeki
wazuri na wenye uwezo mkubwa sana kwa kukaba, ila kwenye idara hii siku
zote Kessy ni bora zaidi ya Juma Abdul kitu kinachomfanya kuwa bora sana
akiwa uwanjani pale timu inaposhambuliwa.
Watu bado wanajiuliza watachezaje vijana hawa wawili kwenye timu
moja, lakini si ajabu Pluijm akaamua kumsogeza mmoja mbele kucheza kama
winga kama ambavyo Jackson Mayanja alikuwa akimtumia Kessy wakati
mwingine alipokuwa Simba.
Hivyo, huwezi kukosea ukisema Pluijm ndiye anajua atawatumiaje hawa
mabeki wawili, lakini kiukweli Kessy vs Abdul mbona patachimbika!
No comments