Tupashane Habari 24-hours

Tupashane Habari 24-hours

Breaking News

kampa kampa tena

YANGA WALIKUWA ‘JAMVI LA WAGENI’ 1998, SASA WATAKUWA WABABE WA AFRIKA

IMG_0078
Na Baraka Mbolembole
Mabingwa mara mbili mfululizo wa ligi kuu Tanzania Bara, timu ya Yanga SC imekuwa timu ya kwanza Afrika Mashariki (Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi) kufuzu kwa hatua ya makundi katika michuano ya Shirikisho Afrika.
Yanga ilikuwa timu ya kwanza pia ukanda huu kufuzu kwa hatua ya makundi ya ligi ya mabingwa Afrika mwaka 1998. Ni wa kwanza katika kila kitu na licha ya kupoteza game ya marejeano jana Jumatano huko mjini Dundo, Angola dhidi ya wenyeji wao Esperanca, mabingwa hao mara 26 wa kihistoria Tanzania Bara wamefanikiwa kukata kiu ya mashabiki wao na wadau wa kandanda Tanzania ambao wamekuwa wakilalamika namna klabu ya VPL zinavyoshindwa mapema katika michuano ya CAF kila mwaka.
Timu ya mwisho ya Tanzania na Afrika Mashariki kufuzu kwa hatua ya makundi ya michuano ya CAF ni Simba SC ambayo inakumbukwa namna walivyowavua ubingwa wa ligi ya mabingwa Zamalek ya Misri na kufuzu kwa hatua ya makundi mwaka 2003. Miaka 13 Leo, Yanga wamefanya hivyo tena, japokuwa safari hii ni katika michuano ya Shirikisho.
Wakati ule (1998) walipofuzu hatua ya makundi kwa mara ya kwanza katika ligi ya mabingwa, Yanga walipangwa katika kundi moja na Asec Mimosas ya Ivory Coast, Manning Rangers ya Afrika Kusini, na Raja Casablanca ya Morocco. Kwa wakati huo, Asec na Raja zilikuwa timu tishio sana katika michuano ya CAF hivyo Yanga ni kama waliangukia katika ‘kundi la kifo’ na kilichowakuta katika michezo 6 ya makundi hawapendi kabisa kukikumbuka.
Waliishia kupewa jina ‘Jamvi la Wageni’ kwa maana game yao ya kwanza tu dhidi ya Raja walikutana na kipigo cha ‘mbwa mwizi’ kutoka kwa Raja baada ya kuchapwa 6-0, Casablanca, wakapigwa 3-0 na Asec katika uwanja wa Uhuru, wakaenda Afrika Kusini wakapigwa 4-0 na Manning Rangers.
Walipoteza pia ugenini 2-1 dhidi ya Asec. Matokeo 1-1 dhidi ya Manning na 3-3 dhidi ya Raja katika uwanja wa Uhuru yalikuwa mazuri zaidi kwao katika michezo 6 ambayo walimaliza wakiwa wameruhusu magoli 19 na kufunga magoli matano tu. Hili halitajirudia na Yanga haitakuwa tena ‘jamvi la wageni’ katika michuano ya CAF.
FUS Rabat, Kawkab Marrakech zote za Morocco, Etoile du Sahel ya Tunisia, Ahli Tripoli ya Libya na MO Bejaia ya Algeria, Medeama ya Ghana na TP Mazembe ya Jamhuri ya DRC ni timu nyingine 7 ambazo zinasubiri kupangwa katika makundi mawili ya michuano hiyo. Yanga imepiga hatua sana ndani ya uwanja, katika utawala na mashabiki wanatembea kwa majigambo kwa kuwa wanaona kazi inayofanywa na timu yao.
Yanga SC ilikuwa ‘jamvi la wageni’ 1998, sasa watakuwa wababe wa michuano kwa maana wana timu nzuri, kocha mzuri, uongozi mzuri, na timu kiumjumla ni bora. Yanga haitaishia hatua ya makundi tu, imani yangu ni itasonga mbele zaidi ya hapo na watavunja rekodi zao wenyewe. Hongera sana Yanga SC kwa kufuzu hatua ya makundi Shirikisho Afrika.
 
Source: 

No comments