Tupashane Habari 24-hours

Tupashane Habari 24-hours

Breaking News

kampa kampa tena

Inawezekaje wasanii kujiita kioo cha jamii kwa Tungo zilizojaa matusi?




Inawezekaje wasanii kujiita kioo cha jamii kwa Tungo zilizojaa matusi?


 Na Abdiel Sifi, OUT

Sanaa ya muziki Tanzania ina historia ndefu, ukichunguza kuchimba na asili yake.

Muziki na wasanii wamepitia mabonde na  milima. Kabla ya uhuru, baada ya uhuru, na wakati huu wa sayansi na teknolojia ya mawasiliano inayochanua kwa kasi. Ndivyo vipindi iliyopitia sanaa ya muziki na ilipo sasa.

Yafaa kuelewa neno Mwanamuziki maana yake.Mtu mwenye uwezo wa kuimba, kutunga mashairi, kutumia vyombo vya muziki, kucheza nk. Ingawa si lazima kwa mtu kuwa na uwezo katika nyanja zote hizo.Aghalabu ajue kutumia moja wapo  ya chombo cha muziki kama kupiga ngoma, filimbi, gitaa, Tarumbeta nk.

Haileti mantiki mtu kuitwa mwanamuziki ili hali hajui kutumia hata chombo mojawapo cha muziki. Haiwezekani mwanajeshi akaitwa mwanajeshi kwa kuvaa sare tu, bila kupitia mafunzo ya jeshi, kutumia silaha,Mpaka awe amepitia mafunzo ndipo huitwa Mwananajeshi, muziki pia inatakiwa hivyo.

Muziki wa tangu uhuru,mfumo wa vyama vingi, hadi leo unatoafautiana sana katika uimbaji, utunzi wa mashairi, upigaji na maudhui yake.

Wasanii wa kitambo muziki wao ulilenga kuelimisha jamii, kuburudisha, kuonya, kukemea, kutoa tahadhari, lakini maisha yao hayakuwa na hadhi kama wanamuziki wa leo.

Tofauti na sasa ambapo msanii anaimba  matusi, kejeli, dharau, kujisifu,akiwa hawezi kutumia chombo  chochote cha muziki na kudiriki kujiita Mwanamuziki, ingawa hajui kupiga ngoma ambayo ni  asili ya makabila ya Kitanzania.

Makala haya yanalenga kujadili zaidi Maudhui ya nyimbo zinazoimbwa kila siku na wasanii wanaoongezeka kama uyoga ulioota kwenye pori la rutuba nyingi.

Haipiti siku bila kusikia wimbo na msanii mpya akichomoza. Hata hivyo nyimbo na wasanii wanaochomoza gizani na kuangaza kwa muda tu, nyota zao huzimika kama moto wa mshumaa. Kuzimika kwao kuna sababu mbalimbali ikiwa kutunga nyimbo zisizosadifu maadili ya kitanzania ,utamaduni na hali ya maisha halisi ya Kitanzania.

Kwa mtu mwenye busara na maadili inamuwia vigumu kukaa kitako na watoto wake, kuangalia video ya bongo flava, kutokana na maudhui na picha zinazoonekana kujaa matusi,mapenzi kejeli na dharau.Itamlazimu haraka kubadili  kituo,kisa! Wimbo umesheheni matusi, dharau, kejeli. Nk.

Sio siri nyimbo, video za bongo flava zimejaa matusi, majigambo na mapenzi, ambapo wasanii hujisifia wao na wapenzi wao ilihali wazazi  (jamii) ina hali ngumu ya maisha, afya duni, ujinga,elimu duni,njaa, maradhi, ufisadi nk. Sina lengo la kuwaelekeza vitu vya kuimba la hasha!.Msanii ni kioo cha jamii ndio wanavyosema wao.Ikiwa hivyo  kwanini  wanashindwa kutazama jamii yao, kujua na kutambua mahitaji  yanayoikabili jamii yao?

Hapo nyuma wanamuziki waliimba nyimbo za kuelimisha jamii, kuonya na kukemea uvivu, ujinga, kuchochea bidii kwa vijana, kujitambua, kupenda nchi yao (uzalendo) kuhamasisha utalii na utunzaji wa mazingira.

Tuangalie nyimbo chache kati ya nyingi zenye maudhui adhimu kwa jamii.Wimbo  Dr Remi Ongala unaitwa Tanzania, una mashairi haya “mwaume ni kilimo,mwanaume ni jembe, lima vizuri watoto wako watashiba, mke wako hataombaomba”.Wimbo  unahimiza watu kufanya kazi kwa bidii (kulima) ili kuepuka njaa katika familia. Na ikiwa wanaume wote watafanya hivyoTanzania itajikwamua katika njaa, umaskini yaani Tanzania hitakuwa omba omba.

Wimbo wa Baraka Mwishehe unaoitwa mama watoto, anasema “baba watoto nashindwa nyamaza naona mambo yananitatiza, tabu na raha ndio hali ya dunia lakini tabu nyingine tunajitakia”.Mashairi yanatoa tahadhari juu ya nidhamu ya matumizi ya mali nyumbani. wanaume kuchukua tahadhari katika familia. “Mwenzangu Weka akiba”.Elimu juu ya watu kutambua wajibu kwa familia, malezi bora kuweka akiba,kwa ajili ya watoto,ndiyo ujumbe uliochagizwa hapa.

Juwata band na wimbo wasia kwa watoto. “Wakati wa ujana wangu, mimi baba yenu, shati dukani shilingi sita dukani unapata, kwa sasa shilingi sita haupati hata mkate/soda. Kuishi kupatana na wakati, jiepusheni na anasa, fanyeni kazi kwa bidii, kama kuna mkorofi kati yenu aache mara moja”. Hakika hawa  wazee walieneza elimu, nasaha murua kwa vijana kuhusu maisha yanavyobadilika. Tahadhari, kuwa makini na muda na kujitambua kutimiza wajibu wa kijana katika maisha.

Linganisha na mashairi ya Nay wa Mitego nakula ujana,  wananita popo nakesha nakula ujana, kujirusha daile sina wikiendi.leta pombe akimwaga tena tumgonge, na demu wake tumuibe. Nataka mademu mabonge wemamba nimewapa likizo.

Mashairi ya wimbo huu yanahamasisha vijana kutumia pesa ovyo bila kujali. Yanachochea vijana kuendekeza starehe badala ya kazi.

Tazama video ya wimbo huu kwa makini, utawaona, hao wanajiita wasanii kioo cha jamii, wakinywa pombe, wanamwaga, pembeni kuna dada zetu waliobarikiwa na Mungu wamevaa chupi wakimshikashika Nay Wa Mitego huku wakiwa katika furaha ya ajabu.



Swali la kujiuliza  ni busara watanzania kuonesha uchi wao hadharani? Je Baraza la sanaa kazi yao ni nini? Video hizi zilizokosa maadili na staha hawazioni? Miaka kadhaa baadaye kutakuwa naTaifa lenye watu wa maadili ya namna gani?



Hotuba ya uzinduzi wa Jamuhuri ya Tanganyika tarehe 09.12.1962, Mwalimu

Julius Nyerere,pamoja na masuala mengine, aliongelea kuhusu historia ya

utamaduni wa Tanganyika.



“Nchi isiyokuwa na utamaduni

wake haina tofauti na mkusanyiko wa watu ambao hawana roho iwawezeshayo kuwa

taifa”. Alivilaani vitendo vya wakoloni vya kuwafanya Waafrika waamini kwamba

hawana utamaduni wao wenyewe; ama kuufanya utamaduni wa Kiafrika uonekane

kitu cha ovyo.



Kutokana na hili, wengi wa waliokuwa wamesoma na kupata elimu ya

Kizungu waliojiona kuwa ni “wastaarabu” walijifunza kuwaiga Wazungu kiasi

kwamba kuwa Mwafrika msomi kulimaanisha kuwa Mzungu Mweusi. Suala la

muziki, kama nyanja muhimu ya utamaduni katika historia ya Tanzania, limekuwa

ainisho muhimu la migogoro ya kitamaduni.



 Mwalimu Nyerere katika hotuba hiyo alizungumzia juu ya  elimu ya kikoloni, kwamba waliopata elimu hiyo  walifunzwa kuimba nyimbo za Kizungu, lakini siyo za Wahehe au Wanyamwezi. Walifunzwa kucheza“rumba”, “chachacha”, “rock ‘n’roll”, “twist, “waltz” na “Foxtrot”. Lakini wengi

walikuwa hawajawahi kucheza au hawakujua chochote kuhusu “Gombe Sugu”,

“Mangala”, “Nyang’umumi,” “Kiduo”, “Lele Mama”, au “Mganda.” Wengi wa

waliosoma wakati wa ukoloni walijua kupiga gitaa au piano, lakini walikuwa hawajui

kupiga ngoma.

Haya yalitamkwa 1962, wakati ambapo kulikuwa hakuna mitandao ya kimawasiliano, video wala televisheni, kama ilivyo leo hii.Pamoja na mandeleo haya muziki waTanzania umepoteza dira, kupotea kwa utambulisho wa muziki wa kitanzania kama sehemu ya utamaduni. Badala yake wasanii huimba matusi, kujisifu na kujifananisha na wazungu, ambapo kweli yake haimo.

Kwa ujumla zipo nyimbo nyingi za wanamuziki wa zamani ambazo kusudi lake lilikuwa kuelimisha jamii,kuburudisha, kutahadharisha.Wanamuziki walijua kutunga mashairi yenye ujumbe murua, walijua kupiga vyombo vya muziki. Mpaka leo nyimbo hizo zikipigwa utatingisha kichwa ishara kuwa unaridhika na mashairi au upigaji wa vyombo vya muziki.

Leo muziki umejaa matusi, unaoshabikia uzembe kwa vijana, kupenda starehe, anasa, ili hali vipato vyao haviwezi  kumudu hali hiyo. Wasanii ni wasanii kweli, waongo, wanaigiza maisha ya uongo. Usasa umetawala. Tukumbuke kuwa muziki ni sehemu ya utamaduni wa Taifa.

Tazama muziki wa kihindi,kijamika,kibrazili kongo Kinshasa nk, ni muziki wa asili yao. Vipi kwetu. Asili ya muziki wa kitanzania ni ipi? Mungu ailaze roho ya Bi Kidude aliyekuwa Mwanamuziki mashuhuri Afrika mashariki. alitangaza muziki wa  asili ya ukanda wa Pwani nje ya Afrika na alipendwa na kuheshimika kitaifa na Kimataifa.

Licha ya udhaifu wa maudhui ya nyimbo za bongo flava, muziki unazidi kupoteza asili na utamaduni uliojaribiwa kujengwa miaka ya 1961/90.Sababu ni kuiga na kuchanganya kila kitu kutoka kwa wengine na kuacha vya kwetu.

Nyimbo za wasanii wa leo kama nilivyosema awali zimajaa matusi, mapenzi, zinazoshabikia uzembe, ujinga. Haumfundishi  mtoto chochote,Kibaya zaidi watoto wanasikiliza na kuzikariri nyimbo hizi  mpaka mwisho, kumzidi hata mtunzi, kuliko kukariri masomo achilia mbali kuelewa. Miaka  mitatu iliyopita baraza la mitihani lililamika wanafunzi  kuandika mistari ya nyimbo za bongo flava wakikujibu mtihani wa kumaliza kidato cha nne.Si dalili nzuri, kizazi kinapotoka, hatua mathubuti zinahitajika kuondoa uozo huu.

Hayo ndiyo matokeo ya muziki wa bongo flava, umewaingia watoto ubongoni  na kuwageuza magogoi, mbumbumbu, wajinga wasio na fikira, waliokata tamaa,wasio na adabu, maadili,utii ujasiri,waoga,waliokosa uzalendo kwa nchi yao.

Wasanii fikira zao wamezielekeza katika mapenzi zaidi, bila kuelewa jamii inakabiliwa na changamoto nyingi zinzohitaji kukemewa,na kutahadharisha jamii. Magonjwa, rushwa na ufisadi ni baadhi yake.

Wasanii wachache wanaothubutu kuhamasisha jamii juu ya utunzaji wa mazingira, mali asili, nidhamu kwa watoto, na kuhamasisha utalii wa ndani na wa nje kama alivyofanya mwanamuziki Nguli Baraka mwishehe kwa wake wimbo unaitwa watalii. Anasema, Tanzania ndio nchi peke yenye wanyama wengi wa kuvutia, watalii kutoka ng’ambo mwakaribishwa mje kuona mengi mnaporudi kwenu mkasimulie.

Hakika muziki wa Mwishehe ulijaa mafundisho  kwa watu wote, kuitangaza nchi yetu,mbuga za wanayama na mali asili alizisifu na kutoa hamasa kwa wananchi kutambua umuhimu wa mazingira asilia. Kupenda nchi, na kutahadharisha vijana kuwa na maadili mema.

Wakati maendeleo ya teknolojia ya mawasiliano yanaendelea kuchipua matawi kwa kasi hapa kwetu, ni vyema mamlaka husika y usimamizi wa sanaa ya muziki (BASATA), ikawasha sigara isiyozimika ili kumulika maudhui ya nyimbo za bongo flava.

Kinachokubalika ni kwamba muziki wa bongo flava umekuwa ajira kwa vijana, unawapatia mafanikio makubwa kimaendeleo.Wakati wakiendelea kusherehekea maendeleo yao ni vyema wakajua kuwa Taifa na jamii linawatazama kama nguzo muhimu kujenga maadili na kuipa mwelekeo jamii yao.

Mamlaka na jamii inapofumba macho halafu wakisiliza na kushabikia mambo ya kijinga ni wazi kuwa tumepoteza dira na tumeshindwa kuhifadhi asili na maadili ya kijamii.

Video za bongo fleva zinazokinzana na maadili ni muhimu pia kumulikwa, ili zile zinazosadifu uongo, ujinga, ngono, na tamaduni za nje zikachukuliwa hatua, ikiwemo kufungiwa na faini. Kama hilo haliwezekani basi mamlaka husika itangaze kwa umma mchana kweupe kwamba “Tanzania ni nchi isiyokuwa na utamaduni wake na ni mkusanyiko wa watu ambao hawana roho iwawezeshayo kuwaTaifa”.



 Makala haya Yameandikwa na Abdiel Sifi

Kwa msaada wa Mtandao


simu 0682 102 671

No comments