Tupashane Habari 24-hours

Tupashane Habari 24-hours

Breaking News

kampa kampa tena

SIMBA VS YANGA Huku mlokole Mwanjali, kule mbabe Bossou

NA ZAITUNI KIBWANA
HOMA ya mpambano wa watani wa jadi, Simba na Yanga unaotarajiwa kuchezwa Oktoba mosi, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, imezidi kupanda ambapo kila timu imejipanga kivyake kuhakikisha inaibuka kidedea siku hiyo.
Kuelekea katika mchezo huo, makocha wa pande zote, Joseph Omog wa Simba na Hans van der Pluijm wa Yanga, wamekuwa wakisuka vikosi vyao kwa lengo la kupata matokeo mazuri na kuwafurahisha mashabiki wao.
Katika mpambano huo safu ya ulinzi kwa pande zote ndiyo inayoweza kuamua matokeo ambapo Simba wanajivunia kuwa na Method Mwanjali ambaye amecheza michezo yote sita iliyopita kwa ustadi mkubwa, huku Yanga wao wakijivunia Vincent Bossou, ambaye hana masihara anapokutana na washambuliaji wa timu pinzani.
Kwa ujumla mpaka sasa vikosi vya pande zote vimekamilika na hakuna timu ambayo ina mchezaji muhimu mwenye majeraha ambaye anaweza kuukosa mchezo huo mbali na Godfrey Mwashiuya wa Yanga ambaye amekuwa majeruhi wa muda mrefu ambapo kazi itakuwa kwa makocha kuamua nani aanze na nani aanzie benchi.
Katika kikosi cha Simba, idadi kubwa ya wachezaji wapo fiti na ni wazi nafasi ya Vincent Angban langoni ipo wazi na kama kutakuwa na tatizo lolote anaweza akapangwa Manyika Peter, huku Yanga wakijivunia Ali Mustafa ‘Barthez’ na Deo Munishi ‘Dida’.
Mpaka sasa kipa wa Simba, Angban ameruhusu mabao mawili na ni kipa ambaye tatizo lake kubwa ni kwamba si mzuri sana wa kuokoa mipira ya krosi ikiwamo kona tofauti na akina Barthez na Dida wa Yanga.
Kwa upande wa beki wa kulia Simba inao Javier Bukungu, Malika Ndeule pamoja na Hamadi Juma ambao wote wanatajwa kutokuwa na kasi kubwa ya kupandisha mashambulizi na kurudi haraka kuokoa kama ilivyo kwa Juma Abdul na Hassan Ramadhan ‘Kessy’ wa Yanga.
Simba wanajivunia kuwa na Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ kushoto huku Yanga nao wakiwa na Haji Mwinyi, ambapo wote hao kazi yao inaonekana huku mabeki wa kati shughuli ikiwa pevu ambapo Yanga wanajivunia Bossou, Kelvin Yondani, Nadiri Haroub ‘Cannavaro’ pamoja na Andrew Vincent ‘Dante’, Simba wao wakiwa na Mwanjali, Novaty Lufunga na Jjuuko Murushid.
Huenda Pluijm akawatumia Bossou na Dante kwani wameonyesha uelewano mkubwa huku Omog akiumiza kichwa kati ya Lufunga na Jjuuko nani anacheza sambamba na Mwanjali ambaye amekuwa nguzo kubwa ya Simba.
Safu hii ya ulinzi ya Simba imeruhusu mabao mawili huku ile ya Yanga ikiruhusu kufungwa bao moja dhidi ya Stand United mchezo uliopita walipopoteza mchezo huo kwa kufungwa bao 1-0.

No comments