Tupashane Habari 24-hours

Tupashane Habari 24-hours

Breaking News

kampa kampa tena

MGOSI ASTAAFU SOKA


Mshambuliji na nahodha wa kikosi cha Simba SC Mussa Hassan Mgosi
MSHAMBULIAJI mkongwe na nahodha wa Simba SC, Mussa Hassan Mgosi amestaafu rasmi soka na sasa anakuwa Meneja wa timu hiyo.
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano ya Simba SC, Hajji Manara amethibitisha hilo na kusema Mgosi ataagwa rasmi katika mchezo wa kirafiki kwa kimataifa utakaopigwa Jumapili ya juma hili uwanja wa Taifa Dar es Salaam dhidi ya URA ya Uganda.
Manara ameeleza kwamba aliyekuwa Meneja wa timu, Abbas Suleiman Ally anakuwa Mratibu wa timu (Team Coordinator) kuanzia leo na nahodha mpya ni Jonas Mkude.
Aidha, kiungo wa klabu hiyo,  Peter Mwalyanzi aliyesajiliwa msimu uliopita akitokea timu ya Mbeya City FC, ametolewa kwa mkopo African Lyon iliyopanda kucheza ligi Kuu msimu huu wa 2015/2016.
Simba wataingia kwenye mechi na URA wakiwapa nafasi mashabiki wao kukiona kikosi chao kwa mara ya pili uwanja wa Taifa baada ya Agosti 8 mwaka huu siku ya Simba Day kuichapa 4-0 AFC Leopard ya Kenya.
Inaelezwa mechi na URA itakuwa ya mwisho  ambapo Agosti 20 wataanza ligi kuu kwa kuchuana na Ndanda FC uwanja wa Taifa.
Lakini wakati huouo mtandao wa habari za michezo Mpenja Sports umeripoti kwamba, mshambuliaji huyo wa zamani wa timu ya taifa Taifa Stars, amekanusha taarifa za kutundoka daruga.
MPENJA SPORTS imemtafuta Mgosi na kumuuliza juu ya taarifa hizo na maelezo yake ni haya: “Kwanza napenda kukanusha suala lililoandikwa kwenye mitandao la Mgosi kustaafu, Mgosi kama Mgosi, suala la kustaafu mpira bado sana, Pogba (Paul) atakapostaafu ndipo atafuatia Mgosi kustaafu”. Amesema Mgosi na kuongeza”
Hata hivyo, Mgosi ameonesha wazi yuko tayari kufanya kazi yoyote ndani ya Simba hata kama atakuwa nje ya uwanja, kitu kinachoashiria yuko mbioni kutundika daluga.
“Mimi ni mchezaji wa Simba, ni Mfanyakazi wa Simba, nipo tayari kufanya majukumu yoyote yanayoihusu Simba, aidha katika uchezaji au sekta nyingine.”
Mgosi anayeheshimika ndani ya Simba amesema kutekeleza majukumu mengine nje ya kucheza ndani ya Simba alishaanza msimu uliopita, lakini hakuna aliyehusisha na kustaafu soka.
“Kuisaidia Simba nje ya uwanja nimelifanya hilo toka mwaka jana, lakini mbona halijaandikwa hivyo, mwaka jana nimekuwa msaidizi wa Mayanja (Jackson), nilimsaidia kila kitu kama kocha msaidizi”. Amesisitiza Mgosi na kufafanua: “Unapozungumza mtu kistaafu tuwe na subira, lazima niseme mwenyewe, sio mitandao iandike, wengine wanaandika wapate comments, likes na kushtusha watu ambao wananihitaji.”
MPENJA SPORTS imemuuliza kama anaamini muda wa kustaafu umefika na yuko tayari kuwa Meneja wa Simba.
“Sio tatizo,  ni jukumu ambalo nitalifanyia kazi kwa vile ninavyofahamu mimi, ukitaka kuangalia kiongozi anayeweza kuingoza Simba kwa kila kitu, hakuna mtu ambaye kwa haraka unaweza kumuangalia zaidi ya Mgosi,  kwasababu ni mtu ninayeheshimika na wachezaji, naheshimika na mashabiki, naheshimika na viongozi wa Simba, naamini katika sekta yoyote nitakayopewa Simba, hakuna atayepinga, kwahiyo najivunia klabu yangu ya Simba,” ameongeza Mgosi.
Licha ya kakanusha kustaafu rasmi, taarifa za ndani ambazo MPENJA SPORTS imezipata ni kuwa kweli Mgosi anaelekea kustaafu na mechi ya Jumapili dhidi ya URA itakuwa maalum kwake kuagwa, lakini yeye mwenyewe na uongozi hauko tayari kulizungumzia kwasababu kuna masuala kadhaa wanajadiliana.
Inaelezwa keshokutwa Jumamosi, Mgosi atakutana  na viongozi wa Simba kujadili suala la nafasi wanayotaka kumpa ikiwemo kuandaa mkataba .

No comments