YANGA NI KUAMUA TU KAMA WALIVYOAMUA, NJIA NYEUPE NUSU FAINALI CAF
Na Baraka Mbolembole
Wawakilishi wa Tanzania katika michuano ya vilabu barani Afrika, timu
ya Yanga SC imepangwa kundi A katika michuano ya kombe la Shirikisho
Afrika 2016 kufuatia ‘draw’ iliyofanyika jana Jumanne huko Cairo, Misri.
Mabingwa mara tano wa ligi ya mabingwa (1967, 1968, 2009, 2010 na
2015) ambao pia ni mabingwa mara moja wa kombe la Shirikisho (1980) timu
ya TP Mazembe ya DR Congo.
Mabingwa mara moja wa ligi kuu ya ridhaa Algeria(2010/11) na washindi
wa FA Cup msimu uliopita, timu ya Mouloudia Olympique de Bejaia ya
Algeria na timu iliyoanzishwa mwaka 2002, Medeama Sporting Club ya Ghana
ndizo zimepangwa na Yanga katika kundi moja.
Kundi ambalo si rahisi kwa mabingwa mara mbili mfululizo wa Tanzania
bara, lakini halitakuwa na ugumu na uzoefu wao wa kucheza zaidi ya mara
20 michuano ya mabingwa Afrika utawavusha na kufika hatua ya nusu
fainali.
Hili ni kundi rahisi zaidi kwa Watanzania kuona timu yao ikiangukia,
na kama kiwango cha msimu huu kitaendelea kuonekana hata hao ‘Bora
Kuliko Mazembe’ wataangusha pointi kwa kikosi cha Hans Van der Pluijm
ambacho kinaweza kushinda taji lake la 3 ndani ya miezi kumi kama
wataifunga Azam FC katika mchezo wa fainali ya kombe la FA siku ya leo
Jumatano.
Yanga ilianza msimu wa 2015/16 kwa kutwaa taji la Ngao ya Jamii,
kisha wametwaa VPL mwezi huu, watafunga msimu leo wakiwa tayari na
tiketi ya kucheza michuano ya klabu bingwa mwaka ujao.
Yanga inaweza kushinda ugenini dhidi ya MO Bejaia timu ambayo
inacheza kwa mara ya kwanza michuano hii tena wakiwa kama mabingwa
wa FA (si timu 3 zilizomaliza katika juu ya msimamo katika ligi kuu ya
Algeria.)
Yanga haijawahi kupata ushindi ugenini dhidi ya timu ya Kiarabu,
lakini wanapaswa kutumia uzoefu tu ili ‘kuvunja mwiko’ huo na MO Bejaia
ndiye nawaona Waarabu wa kwanza kukutana na kipigo cha Yanga wakiwa
kwao. Mguu katika hatua ya makundi utakuwa kwa Wa-algeria hawa wageni
kimataifa.
Nini cha ziada kinachotakiwa? Ni timu kiujumla, wachezaji, benchi la ufundi, uongozi-WAKIAMINI-WAKIPAMBANA-WANAWEZA.
Hili ni kundi jepesi kwa Yanga na TP kwa maana timu hizi zilitolewa
katika michuano ya klabu bingwa hatua ya 16 bora, wakati timu za MO na
Medeama ni mabingwa wa FA katika nchi zao. Simaanishi kuwa hazina ubora,
lakini hata kama wanao hauwezi kuwa tishio kwa Yanga au TP ambazo kila
mmoja atakuwa anatazama namna ya kushinda mechi ya nyumbani
watakapokutana.
Vita ya nafasi mbili za juu, kiuzoefu na ubora, TP na Yanga itawahusu
zaidi kwa maana Mazembe wamekwisha cheza fainali 7 za Champions league,
moja ya klabu bingwa ya dunia, na moja ya Shirikisho Afrika, wakati
Yanga yenyewe imeishia robo fainali 3 za Champions league ( 1969, 1970
na 1998) kati ya mara 21 walizowahi kushiriki katika michuano hiyo.
Kiujumla, Yanga wanacheza kwa mara ya 5 michuano ya Shirikisho hivyo
wana uzoefu ambao wanapaswa kuutumia vizuri ili wavuke hatua ambayo
tayari wamefika safari 3 zilizopita.
Hakuna ugumu kwa Yanga katika kundi hili, ila ugumu unaweza kuwapo
ikiwa Yanga wenyewe watashindwa kupata walau pointi 7 dhidi MO, Medeama
na TP katika uwanja wa nyumbani, na pointi 3 katika game 3 za ugenini.
“Nimeiona ratiba, ni kuamua tu kama tulivyoamua. Ratiba iko poa sana,
nakuhakikishia kwa moto huu tunaenda kufanya vizuri”, aliniambia mlinzi
namba 3 wa timu ya Yanga, Oscar Joshua baada ya kupangwa kwa makundi ya
michuano hiyo.
source


No comments